Last Updated on October 13, 2023 by Dr Mniko
Dawa za Kulevya ni Nini?
Dawa za kulevya ni kemikali ambazo ziingiapo mwilini huathiri ubongo wa mtumiaji na kumsababishia kuwa na matendo, hisia, fikra na muonekano tofauti na matarajio ya jamii.
Kemikali hizi hutokana na mimea na madini ambayo ni mali ghafi muhimu kwa mahitaji mengine ya mwanadamu. Dawa hizi huingia mwilini kwa njia kuu tatu:
- Njia ya kunywa/kula
- Kuvuta na
- Kujidunga sindano
Dawa za kulevya ziko ambazo zimeruhusiwa kisheria kama tumbaku na pombe; ambazo hazijaruhusiwa kama bangi, mirungi, cocaine, heroin na mandrax; na zinazoruhusiwa kwa matumizi ya hospitali kama Valium, pethedine, morphine n.k
Sababu zinazofanya mtu Kutumia Dawa za Kulevya
- Kuna sababu nyingi zinazoweza kumfanya mtu kutumia dawa za kulevya; baadhi ni kama vile; Kuiga tabia na kupenda kujaribu kutokana na ushawishi hasa wa kundi rika.
- Kukosa shughuli ya kufanya
- Magonjwa ya akili kama msongo wa mawazo
- Kujiingiza kwenye starehe hasa klabu za usiku
- Malezi mabaya ya kutoka kwa wazazi / walezi
- Maradhi ya kimwili hasa ya muda mrefu
- Mila na desturi mbali mbali
- Msukumo wa maisha ya kisasa
Madhara ya kutumia Dawa za Kulevya
Madhara ya kutumia dawa za kulevya hutegemea aina ya dawa unayotumia , kiasi cha dawa anayotumika, kama una ugonjwa wa akili, umri wa kuanza kutumia na muda wa matumizi. Yapo madhara ya muda mfupi na muda mrefu.
Madhara ya Muda Mfupi;
- Kuchangamka sana kuliko kawaida (cocaine na mirungi)
- Kuzubaa, kulegea, kupepesuka au kulala (pombe, heroin)
- Kuchanganyikiwa / kuwehuka (bangi)
- Kukosa usingizi, hamu ya kula na hamu ya kujamiana
Madhara ya Muda Mrefu;
- Kupoteza kumbukumbu,
- Kupoteza nguvu ya uzazi
- Magonjwa ya akili, moyo, ini, mapafu, kiharusi, UKIMWI, magonjwa ya ngozi, utapiamlo nk.
- Kuwa na tabia zisizokubalika kwenye jamii kama vile ukorofi, uongo, udokozi, wizi, chuki, lawama, visingizio, kukwepa majukumu na kukosa busara
- Utegemezi wa dawa za kulevya
Utegemezi wa Dawa za Kulevya
Utegemezi wa dawa za kulevya ni hali ambayo mtumiaji wa dawa hulazimika kutumia dawa kila siku ili kupata starehe na kujimudu. Utegemezi unaweza kuwa wa kisaikolojia au wa kimwili.
Utegemezi wa Kisaikolojia
- Kuhangaika sana
- Kuwa mwoga na mnyonge
- Kutojiamani
- Hasira na wasiwasi
- Kushindwa kutekeleza wajibu
- Mawazo hasi
Utegemezi wa Kimwili
- Kukosa usingizi na hamu ya kula
- Kutetemeka mwili
- Kukosa hamu au kushindwa tendo la ndoa
- Kutokwa jasho
- Kuharisha
- Kushindwa kuongea vizuri
- Kuumwa kichwa
- Kupiga miayo mara kwa mara
Kitu Gani Kifanyike kwa Watumiaji wa Dawa za Kulevya?
Elimu ni kitu cha msingi, watu waelimishwe kuanzia utoto wao ili katika maisha yao wafanye uchaguzi sahihi wakifahamu.
- Tiba sahihi na ya mapema
- Tiba ya kisaikolojia (kujitambua aliko, anapotaka kuwa na kuamua kufanya mabadiliko kwa kutegemea uwezo wake mwenyewe
- Tiba kimwili kutumia dawa za hospitali
- Matibabu kwenye nyumba za upataji nafuu (Sober Houses)
- Ushirikiano kati ya mgonjwa jamii au ndugu na wataalam ni muhimu sana katika matibabu ya watu wanaotumia dawa za kulevya.
Piga vita matumizi ya dawa za kulevya kwani zinaharibu nguvu kazi ya familia na Taifa kwa ujumla
Vyanzo
- KIPEPERUSHI KILICHOANDALIWA NA CHUO KIKUU CHA DAR ES SALAAM – MADHARA YA DAWA ZA KULEVYA Barua pepe: healthcentre@udsm.ac.tz
- https://medlineplus.gov/druguseandaddiction.html
Leave feedback about this