Magonjwa ya ndani ya mwili

UGONJWA WA KISUKARI:Sababu,dalili,matibabu

Last Updated on October 13, 2023 by Dr Mniko

Maelezo ya jumla

Ugonjwa wa kisukari (diabetes) ni ugonjwa unaoleta matatizo ya kimetaboliki ambayo husababisha kuwepo kwa viwango vya juu vya sukari katika damu kwa muda mrefu. Dalili za ugonjwa huu ni pamoja na kukojoa mara kwa mara, kuwa na kiu sana, na kuhisi njaa sana. Bila kutibiwa, ugonjwa huu unaweza kusababisha matatizo mengi. Matatizo haya yanaweza kuwa matatizo ya muda mfupi au matatizo makubwa ya muda mrefu ambayo ni pamoja na ugonjwa wa moyo, ugonjwa wa figo, vidonda vya miguu, na uharibifu wa macho.
Ugonjwa huu hutokea baada ya kongosho kushindwa kuzalisha homoni ya insulini ya kutosha. Insulini husaidia kuingiza sukari kwenye seli za mwili na kwa sababu ya upungufu huu sukari hubakia kwenye damu na kuleta madhara makubwa. Kama seli za mwili zitashindwa kuitikia msisimuo unaletwa na homoni ya insulini Seli za mwili zinaposhindwa kuitikia msisimo unaotolewa na insulini husababisha kisukari pia, hili husababishwa na usugu wa seli kwa insulini.
Kuna aina 3 kuu za ugonjwa wa kisukari:

  • Kisukari aina ya 1 ,husababishwa na kongosho kushindwa kuzalisha insulini ya kutosha kutokana na kupungua kwa seli za beta ambazo huzalisha insulini mwilini. Sababu ya kupungua kwa seli hizi haifahamiki vyema.
  • Kisukari aina ya 2, humpata mtu mwenye seli za mwili zenye usugu kwa insulini, hali hii husababisha seli za mwili kutoitikia vyema msisimuo unaotolewa na homoni ya insulini. Sababu kuu ya kupata aina hii ya kisukari ni unene wa mwili uliopitiliza na mazoezi yasiyotosha.
  • Kisukari cha Ujauzito, aina hii ya kisukari huwapata wanawake wajawazito na baada ya kujifungua hupona kabisa,na mara nyingi hawana historia ya kuwa na ugonjwa wa kisukari hapo awali.

Kinga na matibabu ya kisukari huhusisha kudumisha mlo ulio bora na mazoezi ya mwili ya mara kwa mara kudumisha uzito wa mwili unaofaa. Kisukari aina ya 1 ni lazima itibiwe kwa sindano za insulini. Kisukari aina ya 2 inaweza kudhibitiwa kwa dawa pekee au kwa dawa na insulini. Kisukari cha ujauzito kwa kawaida hupona baada ya mtoto kuzaliwa.
Karibu 90% ya wagonjwa wote wanaougua kisukari wana ugonjwa wa kisukari aina ya 2, na idadi hii inazidi kuongezeka kila kukicha. Ni jambo linalofahamika wazi kuwa ugonjwa wa kisukari unaongeza mara dufu hatari ya mtu kufa mapema.

ugonjwa wa kisukari
Mgonjwa akijitoboa tayari kwa kipimo

Dalili na Ishara za ugonjwa wa kisukari

Dalili za mgonjwa wa kisukari asiyekuwa kwenye tiba ni pamoja na:

  • Kupoteza uzito haraka,
  • Kukojoa sana
  • Kuwa na kiu sana na
  • Kuwa na hamu ya kula sana.

Dalili za aina ya 1 zinaweza kujitokeza kwa haraka sana (wiki au miezi), lakini kwa Kisukari aina ya 2 dalili zinaweza kuchelewa sana, zinaweza kuwepo kidogo au zisiwepo kabisa.
Zifuatazo ni dalili nyingine na ishara zinazoweza kuashiria mwanzo wa ugonjwa wa kisukari, ingawa si maalum kwa ugonjwa huu:

Kiwango cha sukari katika damu kikiwa juu kwa muda mrefu husababisha lenzi ya jicho kuharibika na kusababisha matatizo ya macho pia.

Dalili za dharura za ugonjwa wa kisukari     

Kiwango cha sukari katika damu kinaposhuka sana kinaweza kuwa hatari. Dalili hutofautiana kwa kila mtu. Zifuatazo ni dalili unazoweza kuziona kwa tukio la kushuka kwa sukari kwenye damu lisilo kali sana:

  • Kujihisi vibaya tu
  • Kutokwa kijasho chembamba
  • Kutetemeka na
  • Kuongezeka kwa hamu ya kula

Katika tukio lililo kali sana la kushuka kwa kiwango cha sukari mwilini, athari na dalili huwa  kubwa zaidi, kama vile:

  • Kuchanganyikiwa akili
  • Mabadiliko ya tabia kama vile kuwa mkali au mgomvi
  • Kupoteza fahamu
  • Degedege, na kwa mara chache uharibifu wa ubongo wa kudumu au kifo.

Kama tukio sio kali sana, mgonjwa anaweza kujisaidia mwenyewe kwa kula au kunywa kitu chenye sukari nyingi. Kwa tukio kali linaloweza kusababisha ukapoteza fahamu, unapaswa kutibiwa kwenye kituo cha afya kwa kuongezewa maji maalumu yenye sukari au kuchomwa sindano maalumu inayoitwa ”glucagon”.
Hali nyingine ya dharura inayoweza kuwapata wagonjwa (hasa wenye kisukari aina ya 1)  huitwa ”ketoacidosis”. Tatizo hili la kimetaboliki hutokea kwa sababu ya ongezeko kubwa sana la sukari kwenye damu  na upungufu wa maji mwilini. Hali hii ni ya dharura na husababisha mgonjwa kuwa na dalili zifuatazo:

Tukio jingine la nadra lakini hatari linaloweza kuwapata wagonjwa kisukari ni ”hyperglycemic hyperosmolar state”, tukio hili huwapata zaidi watu wenye Kisukari aina ya 2 kwa sababu ya kupungua kwa maji mwilini.

kisukari
Daktari akimpima mgonjwa kiwango cha sukari

Athari za ugonjwa wa kisukari

Aina zote za ugonjwa wa kisukari huongeza hatari ya kupata matatizo ya muda mrefu. Matatizo haya hutokea baada ya miaka 10-20. Athari za muda mrefu huhusishwa na uharibifu wa mishipa ya damu na kuongeza hatari ya kupata ugonjwa wa moyo na mishipa ya damu. Athari nyingi za ugonjwa wa kisukari hutokana na uharibifu wa mishipa midogo ya damu kwenye macho, figo na neva.

  • Uharibifu wa mishipa midogo ya damu katika retina ya macho husababisha uwezo wa kuona kupungua na hatimaye upofu.
  • Ugonjwa huu pia huongeza hatari ya kupata glakoma, mtoto wa jicho, na matatizo mengine ya jicho.
  • Wagonjwa wa kisukari wanashauriwa kumwona daktari wa macho angalau mara moja kwa mwaka.
  • Kuharibika kwa chujio la figo kunaweza kusababisha protini kuanza kupotea kwenye mkojo, na hatimaye figo kushindwa kufanya kazi vizuri.
  • Wagonjwa wenye figo zilizoshindwa kufanya kazi huhitaji mashine maalumu kuchuja damu badala ya figo (dialysis) au kupandikiza figo.

Ugonjwa wa kisukari mara nyingi huharibu mishipa ya fahamu ya mwili. Mgonjwa huhisi ganzi, maumivu na kutokuhisi maumivu. Wagonjwa wa kisukari wana hatari kubwa ya kupata matatizo ya miguu kama vile vidonda na maambukizi. Inaweza kuwa vigumu kutibu matatizo haya na wakati mwingine unaweza kukatwa sehemu ya mguu ili upone.

Ugonjwa wa kisukari husababishwa na nini ?

Kuna aina kuu tatu za ugonjwa wa kisukari

  • Sababu ya ugonjwa wa kisukari aina ya 1
    • Kisukari aina ya 1 husababishwa na kupungua kwa seli za ”beta” zinazozalisha homoni ya insulini kwenye kongosho, na kusababisha upungufu wa insulini. Kinga ya mwili wa mgonjwa huziharibu seli hizi za ”beta” kwa bahati mbaya, baada ya kuzifananisha na kimelea mvamizi. Kitaalamu hali ya aina hii huitwa ”autoimmune attack”. Hata hivyo, mara nyingi sababu ya kupungua seli hizi haijulikani.
    • Kisukari aina ya kwanza inakadiriwa kuathiri 10%, ya watu wote wenye kisukari duniani. Watu wengi walioathirika na ugonjwa huu huwa na afya njema wanapogunduliwa.
    • Japo kisukari aina ya kwanza huwaathiri zaidi watoto, watu wazima pia hupata ugonjwa huu.
    • Watu wanaorithi jeni zinazoongeza hatari ya kupata kisukari aina ya 1 kama vile HLA, huwa na uwezekano mkubwa kupata ugonjwa huu.
    • Kwa watu waliorithi jeni hizi, kuanza kwa ugonjwa wa kisukari kunaweza kusababishwa na sababu moja au zaidi za kimazingira. Sababu kama vile maambukizi ya virusi fulani au chakula anachokula. Virusi kadhaa vimehusishwa na kusababisha kisukari lakini hadi sasa hakuna ushahidi wa uhakika wa kuunga mkono dhana hii.
  • Sababu ya ugonjwa wa kisukari aina ya 2
    • Kisukari aina ya 2 husababishwa na usugu wa mwili kwa homoni ya insulini. Seli za mwili wa mgonjwa mwenye kisukari aina ya 2 zinakosa uwezo wa kuitikia vyema mchocheo unaotolewa na homoni ya insulini. Japo kwa kiasi kidogo, kuna upungufu wa utengenezaji wa insulini kwa wagonjwa hawa, usugu kwa homoni ya insulini ndio tatizo kubwa.
    • Kisukari aina ya 2, husababishwa na mfumo mbaya wa maisha na urithi wa jeni zenye kubeba kisukari toka kwa wazazi .
    • Sababu kadhaa ni muhimu ili kutokea kwa kisukari aina ya 2 , hii ni pamoja na kitambi, ukosefu wa mazoezi ya kutosha, lishe mbaya na msongo wa mawazo.
    • Mafuta mengi katika chakula pia huongeza hatari ya kupata kisukari. Kula kwa wingi mchele na nafaka zingine zilizokobolewa na kusindikwa huongeza hatari pia.
  • Kisukari cha ujauzito
    • Kisukari cha ujauzito hufanana na kisukari aina ya 2 kwa namna kadhaa; Seli za mwili huwa na usugu kwa insulini, lakini pia utengenezaji wa insulini hupungua.
    • Inatokea kwa asilimia 2-10 ya mimba zote na mara nyingi hupona kabisa baada ya kujifungua. Hata hivyo kua baadhi ya wanawake hubakia na kisukari aina ya 2 hata baada ya kujifungua takribani (5-10%)
    • Kisukari cha ujauzito kinaweza kudhibitiwa vizuri kabisa, lakini mgonjwa anahitaji kuwa mwangalifu na kufuata mpango wa matibabu wakati wote wa ujauzito. Matibabu yanaweza kujumuisha mabadiliko ya mlo, upimaji wa mara kwa mara wa kiwango cha sukari mwilini, na wakati mwingine sindano za insulini.
    • Ingawa ugonjwa huu unaweza kuwa wa muda mfupi, usipotibiwa vizuri unaweza kuharibu afya ya mama na mtoto. Mtoto anaweza kuzaliwa akiwa na uzito mkubwa sana na kuongeza changamoto wakati wa kujifungua.  Anaweza pia kuwa na matatizo ya moyo au matatizo ya mfumo wa neva na misuli.
    • Kiwango cha insulini kinapoogezeka katika damu ya mtoto akiwa tumboni kwa mama, hupunguza uzalishaji wa uteute muhimu ambao huitwa”surfactant’. Utete huu husaidia katika upumuaji, kwa hiyo ukipungua unasababisha mtoto kupumua kwa shida.
Mwanaume akijichoma sindano ya insulini

Homoni ya insulini inadhibiti vipi sukari mwilini?

Insulini ni homoni ambayo husaidia kuingiza glukosi kwenye seli za mwili kutoka kwenye damu. Insulini inapopungua au kunapokuwepo na usugu kwa insulini, sukari hurundikana kwenye damu na kusababisha madhara. Mwili hupata sukari kutoka vyanzo vikuu vitatu: kufyonza chakula kutoka tumboni, kuvunjavunja chakula kilichotunzwa tayari kwenye ini kinachoitwa ”glycogen” ili kutengeneza sukari, au kuvunjavunja vyanzo vingine visivyo wanga vilivyo mwilini kutengeneza sukari ”glycogeogenesis”.
Insulini ina jukumu muhimu la kusawazisha kiwango chya sukari mwilini. Insulini inaweza kuzuia kuvunjwavunjwa kwa ”glycogen” au mchakato wa ”gluconeogenesis’. Insulini inaweza kuchochea sukari kuingia kwenye seli, na inasaidia pia kuchochea uhifadhi wa sukari kwa njia ya ”glycogen” ili kupunguza kiwango cha sukari katika damu.
Insulini inatengenezwa na seli za ”beta”, zinazopatikana kwenye kongosho ili kukabiliana na  ongezeko la sukari kwenye damu baada ya kula. Kiwango cha insulini kinachotolewa na seli za ”beta” hupungua pindi tu kiwango cha sukari katika damu kinapopungua, hii husababisha mwili kuvujavunja ”glycogen iliyotunzwa katika ini ili kutengeneza sukari kufidia upungufu huo. Utaratibu huu wa kutengeneza sukari kutokana na ”glycogen” hudhibitiwa na homoni inayoitwa ”glucagon” ambayo hufanya kazi kwa ukinzani na homoni ya insulini.
Kama kiwango cha insulini hakitoshi, au seli za mwili haziitikii vyema mchocheo wa insulini, au kama insulini yenyewe ina kasoro, sukari haiwezi kuingizwa ndani ya seli za mwili na matokeo yake, sukari hulundikana ndani ya damu na kuleta madhara.
Sukari inapoongezeka kwenye damu, figo hushindwa kuinyonya yote na kusababisha kiwango kidogo kubakia kwenye mkojo na kusababisha mkojo kuwa mtamu. Sukari ikibakia kwenye mkojo, huvuta maji mengi na kusababisha mkojo kuwa mwingi sana. Kwa sababu mgonjwa wa kisuakari anakojoa mkojo mwingi, mwishowe hupelekea upungufu wa maji mwilini. Kwa sababu ya kupoteza maji mengi mgonjwa huanza kuhisi kiu ya maji isio ya kawaida.

Utambuzi wa ugonjwa wa kisukari

Ugonjwa huu hutokea wakati mwili unaposhindwa kudhibiti sukari katika damu, sukari inaporundikana katika damu inaweza kufikia kiwango cha hatari, ili kujua kiwango cha sukari katika damu, vipimo vya sukari hufanyika, na vipimo vifuatavyo huonesha kama mgonjwa ana ugonjwa huu;

  • Kipimo cha sukari kinapoonesha zaidi ya 7.0 mmol/L baada ya kufunga bila kula kwa muda wa saa nane (fasting blood glucose).
  • Kipimo cha sukari kipimwacho wakati wowote (random blood glucose) kinapoonesha zaidi ya 11.1 mmol/L ,huku kukiwepo na dalili zozote za kisukari.

Ukibainika una kiwango cha juu cha sukari katika damu na daktari hajaridhika na majibu, anaweza kupendekeza kurudia kipimo hicho siku inayofuata, itapendeza zaidi kama utafunga kwa muda wa saa nane kabla ya kipimo ili kujiridhisha na matokeo.
Kulingana na shirika la afya duniani, watu wenye kiwango cha sukari kutoka 6.1 hadi 6.9 mmol/L baada ya kufunga masaa manane, wako kwenye hatari ya kupata ugonjwa huu na magonjwa ya moyo.

Daktari akipima kiwango cha sukari kwa glucometer

Jinsi ya kuzuia ugonjwa wa kisukari

Hakuna njia inayojulikana ya kujikinga na Kisukari aina ya 1. Kisukari aina ya 2 huathiri kiasi cha 85-90% ya wagonjwa wote wa kisukari duniani, aina hii inaweza kuzuiwa kwa kupunguza uzito wa mwili, kufanya mazoezi, na kula mlo bora.
Kubadilisha kile unachokula husaidia kwa kiasi kikubwa kuzuia ugonjwa huu. Chagua kula vyakula vya nafaka isiyokobolewa, na epuka kutumia mafuta mengi kwenye chakula, mafuta yanayotokana na karanga, mbogamboga na samaki yanafaa zaidi. Punguza kunywa vinywaji vya sukari na punguza ulaji wa nyama nyekundu. Kuacha kuvuta sigara hupunguza kwa kiasi kikubwa uwezekano wa kupata ugonjwa huu.

Matibabu ya ugonjwa wa kisukari

Ugonjwa wa kisukari hauwezi kutibiwa na kupona kabisa. Mgonjwa anapaswa kutumia dawa za kudhibiti sukari maisha yake yote. Matibabu ya kisukari hujaribu kurudisha kiwango cha sukari katika kiwango cha kawaida. Hii inawezekana kwa kula mlo bora, kufanya mazoezi, kupunguza uzito, na kutumia vyema dawa.

  • Mgonjwa wa kisukari aina ya kwanza anapaswa kutumia insulini pekee. Kamwe hapaswi kutumia dawa nyingine zozote za kudhibiti sukari isipokuwa sindano za insulini pekee.
  • Kwa mgonjwa kisukaria aina ya pili anaweza kutumia dawa za kudhibiti sukari, anaweza kutumia insulini kwa nyakati maalumu kulingana na maelekezo ya daktari au anaweza kutumia vyote kwa pamoja.

Mgonjwa anapaswa kujifunza kuhusu ugonjwa huu na kushiriki kikamilifu katika matibabu ili kudhibiti sukari ipasavyo. Mgonjwa anapaswa kuacha kuvuta sigara, kupunguza kiwango cha lehemu mwilini, kupunguza uzito wa mwili na kufanya mazoezi.

Kufuatilia kiwango cha sukari na mtindo bora wa maisha ni muhimu

Maelezo ya ziada

  • Mfumo wa Maisha
    • Watu wenye ugonjwa huu wanapaswa kupewa elimu kuhusu ugonjwa wa kisukari na matibabu yake, wanapaswa kula mlo bora ili kuweka uzito wa mwili sawa na kufanya mazoezi ya mwili ili kudhibiti kiwango cha sukari mwilini. Kubadili mfumo wa maisha husaidia kupunguza hatari ya kupata magonjwa ya moyo na kudhibiti shinikizo la damu. Hakuna mlo maalumu uliothibitishwa unaowafaa watu wenye kisukari, mlo wowote utakaokula na kufanikiwa kupunguza uzito wa mwili unafaa.
  • Madawa
    • Ukweli usiopingika ni kuwa, mgonjwa anaedhibiti vyema viwango vya sukari katika damu kwa kutumia dawa vyema, hupunguza maradufu uwezekano wa kupata athari mbaya zitokanazo na ugonjwa huu, kwa mfano matatizo ya figo, macho n.k.
    • Kuna makundi kadhaa ya dawa za kudhibiti ugonjwa huu. Baadhi hupatikana kama vidonge, mfano ”metformin”, na zingine kwa njia ya sindano kama vile GLP-1 agonists. Kisukari aina ya 1 hutibiwa kwa insulini pekee.
    • ”Metformin” hupendekezwa kama tiba ya mwanzo ya ugonjwa wa kisukari aina ya 2, hufanya kazi kwa kupunguza uzalishaji wa sukari wa ini. Makundi mengine kadhaa ya dawa hutumika kutibu kisukari aina ya 2,dawa hizi husaidia kuongeza kiwango cha insulini inayotengenezwa mwilini, zingine hupunguza kiwango cha sukari kinachofyonzwa kutoka tumboni, na nyingine hupunguza usugu wa seli kwa insulini.
  • Shinikizo la damu
    • Wagonjwa wa kisukari wanapaswa kudhibiti kiwango cha shinikizo la juu la damu. Wataalamu wanapendekeza kiwango cha juu cha shinikizo la damu kuwa chini ya 130/80 mmHg ili kupunguza uwezekano wa kupata magonjwa ya moyo na kiharusi.
  • Upasuaji
    • Upasuaji wa kupunguza uzito (Weight loss surgery) huwasaidia baadhi ya wagonjwa wenye kisukari aina ya 2. Wengi wao huweza kudhibiti kiwango cha sukari kwa kutumia dawa kidogo au bila dawa kabisa baada ya upasuaji.
    • Japo vifo vya muda mrefu hupungua baada ya upasuaji, 1% ya wagonjwa hufa kutokana na athari za upasuaji. Inashauriwa kuwa kufanyiwa upasuaji iwe chaguo la mwisho kabisa, pale tu mgojwa anaposhindwa kupunguza uzito na kushindwa kabisa kudhibiti sukari chini ya viwango vilivopendekezwa.

Vyanzo

https://medlineplus.gov/ency/article/001214.htm

Leave feedback about this

  • Quality
  • Price
  • Service

PROS

+
Add Field

CONS

+
Add Field
Choose Image
Choose Video
X