Last Updated on October 13, 2023 by Dr Mniko
Maelezo ya jumla
Kushuka kwa shinikizo la damu (hypotension), ni hali ya kuwa na shinikizo la damu lililo chini sana kuliko kawaida. Hii humaanisha moyo, ubongo, na sehemu nyingine za mwili hazipati damu ya kutosha.
Nini dalili za kushuka kwa shinikizo la damu?
Dalili zinaweza kujumuisha:
- Kuona maluweluwe
- Kuchanganyikiwa
- Kizunguzungu
- Kupoteza fahamu
- Kuhisi usingizi
- Uchovu/ Kukosa nguvu
Nini sababu ya kushuka kwa shinikizo la damu?
Shinikizo la damu linaloonekana kuwa chini kwa mtu mmoja linaweza kuwa la kawaida kwa mtu mwingine. Shinikizo la damu la kawaida kwa watu wengi, ni kati ya 90/60mmHg hadi 130/80 mm Hg. Shinikizo la damu likishuka hata kidogo tu, hata kama ni 20mmHg pekee, linaweza kusababisha matatizo kwa watu wengine.
- Kushuka kwa presha kumegawanywa katika makundi matatu:
- Kushuka kwa shinikizo kunakosababishwa na mabadiliko ya ghafla ya mkao au mlalo wa mwili ”orthostatic hypotension” – Mara nyingi humtokea mtu anaposimama haraka kutoka kitandani alipolala. Aina hii ya kushuka kwa shinikizo hudumu kwa sekunde au dakika chache tu. Kama aina hii ya kushuka kwa shinikizo itatokea baada tu ya kula chakula huitwa ”postpandial hypotension”. Mara nyingi, aina hii huwapata zaidi wazee na watu wenye ugonjwa wa parkinson.
- Kushuka kwa shinikizo kunakotokea baada ya kusimama kwa muda mrefu ”neurally mediated hypotension”. Aina hii huwapata zaidi vijana na watoto. Kwa kawaida, kadri watoto wanavyokuwa hali hutoweka.
- Kushuka kwa shinikizo kunakosababishwa na upotevu mkubwa wa ghafla wa damu, maambukizi au matokeo makali ya mzio ”allergic reaction”
- Kushuka kwa presha kunaweza kusababishwa na madawa kama:
- Pombe
- Madawa ya kudhibiti msongo na wasiwasi
- Baadhi ya madawa ya kudhibiti sonona/ kushuka moyo
- Madawa ya kupunguza maji mwilini ”diuretics”
- Madawa ya kutibu moyo, hii ni pamoja na yanayotumiwa kutibu shinikizo la juu la damu na magonjwa ya moyo
- Madawa yanayotumiwa wakati wa upasuaji
- Madawa ya kupunguza maumivu
- Sababu nyingine za kushuka kwa presha ni:
- Kisukari
- Matokeo mabaya sana ya mzio
- Mapigo ya moyo yasiyo sawa
- Upungufu wa maji mwilini
- Kuzirai
Utambuzi wa tatizo la kushuka kwa shinikizo la damu
Mtoa huduma wa afya atakuchunguza na kujaribu kutambua nini kinachosababisha shinikizo lako la damu kushuka. Mtoa huduma atapima joto lako la mwili, mapigo ya moyo, kiwango cha upumuaji wako, na shinikizo la damu. Unaweza kuhitajika kukaa hospitalini kwa muda fulani.
Daktari anaweza kukuuliza maswali yafuatayo:
- Je, shinikizo lako la damu la kawaida ni kiasi gani?
- Je, unatumia dawa gani?
- Je, umekuwa ukila na kunywa kama kawaida?
- Je, Umeumia au kuugua ugonjwa wowote hivi karibuni?
- Je! una dalili nyingine?
- Je! Umezimia au kupoteza fahamu?
- Je! Unahisi kizunguzungu ukisimama au ukiketi baada ya kulala?
Vipimo vifuatavyo vinaweza kufanyika:
- Kipimo cha kupima kiwango cha metaboli ya mwili –basic metabolic panel
- Blood culture – damu hupandikizwa katika mazingira maalumu ya maabara ili kukuza vimelea na kutambua maambukizi kwenye damu
- Complete blood count –hesabu ya seli zilizomo kwenye damu humpatia daktari taarifa mbalimbali –kama kuna maambukizi, mzio au upungufu wa damu
- Electrocardiogram –ni kipimo kinachorekodi umeme unaopita kwenye moyo ili kutambua matatizo ya moyo
- Kipimo cha mkojo –urinalysis
- Eksirei ya tumbo
- Eksirei ya kifua
Wakati gani utafute matibabu ya haraka?
Unapokua na dalili zinazotokana na kushuka kwa shinikizo la damu, unapaswa kuketi chini au kulala mara moja na kuinua miguu yako juu ya usawa wa moyo wako.
Kama kushuka kwa shinikizo kutasababisha mtu kupoteza fahamu, tafuta msaada wa kitabibu haraka. Kama mtu aliyepoteza fahamu hapumui au hana mapigo ya moyo, fanya CPR.
Mwone daktari mara moja kama una dalili zifuatazo:
- Kinyesi cheusi au chenye damu
- Maumivu ya kifua
- Kizunguzungu
- Kuzirai/ kupoteza fahamu
- Homa juu ya nyuzi 38.3℃
- Mapigo ya moyo yasiyo sawa
- Kupumua kwa shida
Mwone daktari kama:
- Unahisi maumivu wakati wa kukojoa au dalili nyingine
- Kikohozi chenye kutoa kohozi
- Unashindwa kula au kunywa
- Unaharisha au kutapika kwa muda mrefu
Uchaguzi wa matibabu kwa tatizo la kushuka kwa shinikizo la damu
Kushuka kwa presha kwa mtu mwenye afya njema mara nyingi hakuhitaji matibabu.
Kama una ishara au dalili za kushuka kwa shinikizo la damu, unaweza kuhitaji matibabu. Matibabu hutegemea sababu ya kushuka kwa shinikizo la damu. Ni dharura ya kimatibabu kama kushuka kwa shinikizo la damu kumesababishwa na mshtuko ”shock”.
Unaweza kuongezewa damu kupitia kwenye mshipa, unaweza kupewa madawa ya kupandisha shinikizo la damu na kuboresha nguvu ya moyo kusukuma damu, na madawa mengine, kama vile antibiotiki.
Kama madawa yanasababisha kushuka kwa shinikizo, kunakosababishwa na mabadiliko ya ghafla ya mkao au mlalo wa mwili ”orthostatic hypotension”, daktari anaweza kubadilisha dozi au dawa. USIACHE kutumia dawa kabla ya kuongea na daktari wako. Matibabu mengine ya aina hii ya kushuka kwa shinikizo ni pamoja na kuongezewa maji kama kuna upungufu mwilini au kuvaa soksi maalumu zinazobana miguu ili kuongeza shinikizo la damu miguuni.
Kwa watu ambao kushuka kwa shinikizo la damu kunakotokana na kusimama kwa muda mrefu (neurally mediated hypotension) wanapaswa kuepuka kusimama kwa muda mrefu. Matibabu mengine ni pamoja na kunywa maji mengi na kuongeza kiasi cha chumvi katika mlo. (Muulize daktari akupe mapendekezo). Katika hali kali, daktari anaweza kuagiza madawa kama vile fludrocortisone yatumike.
Dawa za kuepuka
Wagonjwa wenye tatizo la kushuka kwa shinikizo la damu, wanapaswa kuepuka madawa yafuatayo:
- Verapamil
- Labetalol
- Propafenone
Kama una tatizo la kushuka kwa shinikizo la damu, ongea na daktari kabla ya kuanza au kuacha kutumia dawa hizi.
Kuzuia
Kama una tatizo la kushuka kwa shinikizo la damu, daktari anaweza kupendekeza hatua kadhaa ili kuzuia au kupunguza dalili. Hatua hizi ni pamoja na:
- Kuepuka unywaji wa pombe
- Kuepuka kusimama kwa muda mrefu (kama kusimama ndio chanzo )
- Kunywa maji ya kutosha
- Simama au amka polepole au kwa hatua baada ya kuketi au kulala
- Tumia soksi za kubana miguu (compression stockings) ili kuongeza shinikizo la damu miguuni
Nini cha kutarajia?
Kwa kawaida, tatizo la kushuka kwa shinikizo linaweza kutibiwa kwa mafanikio.
Matatizo yanayoweza kutokea
- Mshtuko
- Majeraha yanayotokana na kuanguka baada ya kuzimia
- Kuanguka ni hatari sana, hasa kwa wazee. Kuvinjika kunakotokana na kuanguka, kunaweza kuathiri ubora wa maisha ya mtu.
- Kushuka kwa shinikizo la damu huupunguzia mwili oksijeni na kusababisha matatizo ya moyo, ubongo, na viungo vingine.
Leave feedback about this