Last Updated on October 13, 2023 by Dr Mniko
Maelezo ya jumla
Mtoto wa jicho (cataract) ni ukungu kwenye lenzi ya jicho unaoathiri uwezo wa kuona. Inaweza kutokea kwa jicho moja au yote, lakini haiwezi kuenea kutoka kwenye jicho moja hadi jingine.
Nini dalili za mtoto wa jicho?
Mgonjwa huwa na matatizo yafuatayo:
- Kuona ukungu kwenye jicho
- Kupoteza uwezo wa kuona rangi vizuri
- Kuona vitu viwili viwili au picha nyingi kwenye jicho moja
- Ugumu kuona usiku
- Kuona miduara ya mwangaza/nuru hasa unapokuwa karibu na taa
- Mgonjwa huumizwa sana na mwanga mkali
Kwa kawaida, ugonjwa huu hupunguza uwezo wa kuona hata wakati wa mchana. Watu wengi wenye ugonjwa huu, huwa na matatizo kwenye macho yote mawili, japo jicho moja linaweza kuwa vibaya zaidi ya jingine.
Nini sababu za mtoto wa jicho?
Mara nyingi, sababu ya kutokea kwake haijulikani. Kwa watu wazima, mtoto wa jicho huanza na kukua taratibu kadri umri unavyoongezeka. Hukua na kuongezeka polepole bila kusababisha maumivu yoyote, na uwezo wa kuona wa jicho lililoathirika hupungua kadri siku zinavyopita. Baadhi ya watafiti wanadhani kuwa, mtoto wa jicho hutokea baada ya protini iliyo kwenye lenzi kuchoka na kuharibika baada ya matumizi ya muda mrefu.
Japo sehemu kubwa ya ugonjwa huu huhusishwa na uzee, aina nyingine huwa na sababu mbalimbali:
- Ugonjwa huu inaweza kuanza baada ya upasuaji kwenye jicho uliofanyika kurekebisha tatizo jingine la jicho, kama vile glakoma. Mtoto anaweza kuanza kwa watu ambao wana matatizo mengine ya kiafya, kama vile ugonjwa wa kisukari. Wakati mwingine huhusishwa na matumizi ya dawa za corticosteroids.
- Mtoto wa jicho baada ya jeraha: Anaweza kutokea baada ya kuumia jicho, wakati mwingine baada ya miaka mingi.
- Kuzaliwa na mtoto wa jicho: Watoto wengine huzaliwa au kutokewa na mtoto wa jichoni utotoni, mara nyingi huwa kwenye macho yote.
- Mtoto wa jicho inayosababishwa na mionzi: Anaweza kutokea baada ya kukutana na aina fulani ya mionzi.
Mtoto jichoni hukua haraka zaidi kama mtu atakuwa anavuta sigara, atakutana na vitu vya sumu, atakaa kwenye mazingira yenye mwanga mkali sana wa jua.
Nani yuko kwenye hatari zaidi?
Hatari ya kupata mtoto wa jicho huongezeka kadri mtu unavyozeeka. Sababu nyingine ni pamoja na:
- Magonjwa fulani kama vile ugonjwa wa kisukari.
- Tabia binafsi kama vile uvutaji wa sigara na matumizi ya pombe.
- Mazingira kama vile kukaa kwa muda mrefu kwenye mwanga wa jua.
Utambuzi wa mtoto wa jicho unafanyikaje?
Uchunguzi wa kawaida wa jicho na uchunguzi wa kutumia kifaa cha kupimia macho ( slit lamp) husaidia kutambua mtoto wa jicho. Mara nyingi vipimo vingine vya uchunguzi havihitajiki.
Uchunguzi wa macho hujumuisha:
- Visual acuity: Kipimo hiki hupima uwezo wa macho kuona kwenye umbali tofautitofauti.
- Dilated eye exam: Matone kadhaa ya dawa huwekwa machoni ili kupanua mboni ya jicho. Mtaalamu wa jicho hutumia lenzi maalum ili kuchunguza retina na neva zilizo jichoni kama kuna ishara za uharibifu na matatizo mengine ya jicho.
- Tonometry: Kifaa maalumu hupima shinikizo ndani ya jicho. Matone ya dawa ya ganzi yanaweza kuwekwa jichoni kabla ya kipimo hiki.
Wakati gani utafute matibabu ya haraka
Mwone mtoa huduma wa afya ukipoteza uwezo wa kuona mchana au usiku.
Uchaguzi wa matibabu ya mtoto wa jicho
Dalili za awali za mtoto wa jicho zinaweza kupunguzwa kwa kuvaa miwani, mwanga bora, kuvaa miwani ili kupunguza mwanga mkali na kutumia lenzi ya kukuzia vitu. Kama hatua hizi hazitasaidia, upasuaji ndio tiba pekee yenye ufanisi. Upasuaji hufanyika ili kuiondoa lenzi iliyoharibika na kuweka lenzi bandia.
Kama mtoto wa jichoni hakusumbui, upasuaji sio lazima. Hata hivyo, watu wengine wanaweza kuwa na matatizo zaidi ya jicho, kama vile matatizo ya retina yanayosababishwa na kisukari, ambayo hayawezi kutibiwa kabla ya upasuaji wa mtoto wa jicho.
Kwa watu wengine, kubadilisha miwani au kutumia lenzi ya kukuza vitu husaidia sana . Upasuaji huhitajika, kama shughui za kila siku zitaathirika, kama vile kuendesha gari, kusoma, au kutazama TV.
Magonjwa yenye dalili zinazofanana
Magonjwa kadhaa yanaweza kuwa na dalili zinazofanana na mtoto wa jicho, hii ni pamoja na:
- Uzee
- Glakoma
- Kisukari
- n.k
Kuzuia
Kuvaa miwani na kofia ili kuzuia mwanga wa jua inaweza kusaidia kupunguza kukua kwa mtoto wa jicho. Kama unavuta sigara, acha. Watafiti wanaamini kuwa, lishe nzuri inaweza kusaidia kupunguza hatari ya kupata ugonjwa unaohusishwa na umri. Wanapendekeza kula mbogamboga, matunda, na vyakula vingine vyenye antioxidants.
Kama una umri zaidi ya miaka 60 au zaidi, unapaswa kufanya uchunguzi wa macho kwa angalau mara moja kila baada ya miaka miwili.
Nini cha kutarajia?
Uwezo wako wa kuona unaweza usirudi kuwa 20/20 kama iivyokuwa mwanzo baada ya upasuaji kama kuna magonjwa mengine ya macho. Dakari anapaswa kukutarifu hili mapema kabisa kabla ya upasuaji.
Leave feedback about this