Magonjwa ya akili

UKWELI KUHUSU ATHARI ZA BHANGI

banghi

Last Updated on October 12, 2023 by Dr Mniko

Maelezo ya jumla

Bhangi ndiyo mhadarati unaotumiwa vibaya zaidi kati ya vijana duniani. Vijana hutumia bhangi kwa sababu nyingi. Huenda waitumie kwa vile wana tamaa ya kujua inavyohisi, kufanana na wenzao au kuwa wa kisasa, au huenda wasukumwe kuitumia na vijana wenzao. Vijana pia wanaweza kutumia bhangi ili kukabiliana na hofu, hasira, mfadhaiko, au uchovu.

Bhangi ni mchanganyiko wenye rangi ya kijani kibichi, kahawia au kijivu, wa majani, mizizi, mbegu na maua ya mmea yaliyokaushwa, kukatakatwa. Majina ya kawaida ya bhangi ni kama: Msuba, ganja, majani, cha Arusha, cannabis, weed, grass, pot, hash, au hashish.

Bhangi huvutwa kwa kuisokota iwe kama sigara (inayoitwa joint) au huvutwa kwenye kiko. Mtu anapovuta bhangi, yeye huhisi athari yake karibu papo hapo, na wao huchukuliwa kuwa “wamelewa.” Kulewa huku husababishwa na kemikali fulani iliyo kwenye bhangi inayoitwa THC, inayoathiri ubongo na sehemu zingine za mwili. Kuna athari nyingi za muda mfupi na mrefu za uvutaji bhangi.

Athari za Muda Mfupi za bhangiBhangi

Katika muda mfupi, matumizi ya bhangi yanaweza kusababisha matatizo yafuatayo mwilini:

  • Hisia nzito ya furaha (kulewa)
  • Ugumu kuzingatia na kuwa makini
  • Kufanya maamuzi yasiyo ya kawaida
  • Kufanya maamuzi ya pupa bila kufikiria
  • Kukosa motisha
  • Matatizo ya kumbukumbu/fahamu
  • Macho mekundu
  • Midomo iliyokauka
  • Hamu kubwa ya kula – unakula sana
  • Mapigo ya moyo yaliyoongezeka
  • Hofu, woga, kutoamini watu, au kushuku watu
  • Matatizo ya usingizi
  • Majeraha yasiyokusudiwa; kama yanayotokana na ajali ya gari

Athari za Muda Mrefu za bhangiMajani ya bangi

Uvutaji bhangi kila wakati au kwa muda mrefu huweza kusababisha matatizo yafuatayo mwilini:

  • Shida za kupumua
  • Kiwango pungufu cha uerevu (IQ)
  • Athari mbaya kwa masomo
  • Kutoridhika na maisha
  • Mfadhaiko/Ugonjwa wa sonona
  • Hofu
  • Fikra za kujiua
  • Shida nyingi za kifamilia, mahusiano kuvunjika

Kweli zingine kuhusu bhangi unazopaswa kujua.

Bhangi inasababisha kufeli shuleni. Utumiaji banghi unaweza kuwa na athari mbaya, na kusababisha kupungua kwa umakini, kumbukumbu/ufahamu, na uwezo wa kujisomea kwa siku au wiki kadhaa—hasa unapoitumia kila wakati. Vijana wavutao bhangi hupata alama za chini sana na huwa na uwezekano mkubwa wa kuacha masomo kuliko vijana wasiovuta bhangi. Utumiaji bhangi unaweza kupunguza uerevu/IQ yako ukiivuta kila wakati katika miaka ya ujana. Watumiaji bhangi kwa muda mrefu huripoti kuridhika kidogo katika maisha yao, matatizo ya kumbukumbu/ufahamu na shida za kimahusiano, afya mbovu ya kimwili na kiakili, mishahara midogo, na fanaka mdogo kitaaluma/kikazi.

Kwa vile bhangi huathiri uamuzi, inaweza kuhatarisha maisha ya watu. Bhangi, sawa na dawa zingine zinazotumiwa vibaya, inaweza  kutatiza uamuzi. Hii huweza kusababisha tabia zenye hatari ambazo zinaweza kumweka mtumiaji kwenye hatari ya kuambukizwa Virusi Vya Ukimwi.

Ni hatari kuendesha gari baada ya kutumia bhangi. Bhangi huathiri ustadi unaohitajika kwa uendeshaji salama—umakini, uangalifu, na uwezo wa kuitikia matukio ya kwa wakati. Bhangi hutatiza uwezo wa kutambua umbali kati ya kitu kimoja na kingine na hupunguza uwezo wa kujibu isha au sauti anapokuwa barabarani. Ukiachilia mbali ulevi wa pombe, bhangi ndio mhadarati unaochangia ajali nyingi zaidi barabarani, ikiwemo zile zinazosababisha vifo.

Unaweza kutawaliwa/uraibu wa bhangi. Siyo kila mtu avutae bhangi hutawaliwa. Hata hivyo, utumiaji bhangi kila wakati huweza kusababisha kutawaliwa. Hii inamaanisha kuwa mtu hawezi kuacha kutumia bhangi ingawa angependa kuacha.

Bhangi inachukuliwa kuwa “mhadarati-mfunguzi.” Watumiaji wa bhangi wana uwezekano mkubwa wa kujaribu, mihadarati inayodhuru afya zaidi katika siku za usoni.

Vyanzo

https://medlineplus.gov/marijuana.html

 

Leave feedback about this

  • Quality
  • Price
  • Service

PROS

+
Add Field

CONS

+
Add Field
Choose Image
Choose Video
X